Pages

MWONGOZO WA MSTAHIKI MEYA

MWONGOZO WA MSTAHIKI MEYA

 SEHEMU I 

 Onyesho I.
 Mchezo uanzapo, tunakutana na Waridi ambaye ni nesi na Siki ambaye ni daktari. Wote wawili wako kwenye zahanati ya Jiji. Daktari Siki anaonekana mwenye kusumbuliwa na jambo fulani; pengine matatizo ya ukosefu wa dawa zahanatini. Waridi aingiapo, wanaanza kuangazia swala la ukosefu wa dawa kwenye zahanati. Waridi anamwambia Siki kwamba, shehena ya dawa iko bahari kuu na kwamba ingewasili baada ya siku tatu. Hii ni kwa mujibu wa Mstahiki Meya mweneyewe. Zahanati ingepokea dawa hizo baada ya siku tatu zingine baada ya kuwasili nchini. Meya anasema wagonjwa wasubiri dawa, naye daktari anashangaa kana kwamba ugonjwa nao utasubiri. Kutokana na mazungumzo ya Waridi na daktari Siki tunagundua kwamba, zaidi ya kukosekana kwa dawa, wagonjwa hawana pesa za kulipia huduma za matibabu. Hata hivyo, amri ni kwamba, lazima wagonjwa walipie huduma za afya kabla hazijatolewa kwao. Waridi anatetea hali hii kwa kusema kwamba nchi yao ni maskini. Siki anapomuuliza mwenye kusema kwamba nchi ni maskini, Waridi anasema kwamba ameyasikia tu maneno hayo kutoka kwa wanasiasa, vyombo vya habari na wasomi. Siki haelekei kukubaliana naye na anashangaa kwamba ‘ameyasikia tu’. (Hii inadhihirishwa kwamba, vyombo vya habari, wanasias na wasomi wanawapotosha wananchi kwamba nchi yao ni maskini.) Pindi anaingia mama mwenye mtoto mgonjwa. Waridi anamkemea lakini Siki anampokea na kuanza kumhudumia. Tunagundua kwamba, mtoto alikula maharage aliyoletewa na mamake kutoka anakofanya kazi; kwa Mstahiki Meya.Tunaonyeshwa hapa kwamba, jamii hii inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa chakula; haswa pale mama huyu anakiri kwamba huwa wanakula chakula cha mbwa bila ‘dhara yoyote’. Zaidi tunaona kwamba, mtoto huyu ana tatizo la utapiamlo; ushahidi wa kuwa pana ukosefu wa lishe bora. Daktari anapendekeza mtoto alazwe kwenye wadi ya watoto na anajishughulisha kumpa huduma kwa kujitengenezea dawa ya mchanganyiko wa sukari na chumvi kwenye maji moto. Anapendekeza pia kwamba, wagonjwa wote waliolemewa walazwe hata ingawa hakuna dawa huku akisema kwamba wakifa watakufa kwa kukosa dawa lakini si kwa kukosa matumaini. Anasisitiza kwa kusema ‘ganga ganga ya mganga huleta tumaini.’ Tunapata kufahamu pia kwamba,wagonjwa hawa ni wafanyakazi wa Jiji husika.. dakatari anasema “…Asasi na wahudumiwa vyote viko chini ya Meya…” akiwa na maana kwamba, hospitali ni ya Jiji na wagonjwa ni wafanyakazi wa Jiji. Inabidi wagonjwa walazwe huku dawa zikisubiriwa. Wakati uo huo Siki anashangaa ni kwa nini Meya akatoa kauli badala ya Bwana Uchumi na Kazi; inaelekea kuna jambo ambalo linaendelea pale na wanakubaliana kusubiri ili waone yatakayotokea. 

Tathmini
Kutokana na onyesho hili tunaona kwamba, jamii hii imezingirwa na matatizo mengi: kwanza kuna tatizo la ukosefu wa dawa kwenye hospitali za umma. Pia kuna tatizo la ukosefu wa uajibikaji miongoni mwa viongozi kama vile Meya. Meya anatoa kauli ambazo hazifai kama vile kwamba ni lazima wagonjwa walipie huduma za afya kabla hazijatolewa kwao. Vile vile, kuna kutojali hali ya wananchi na haswa wagonjwa, wanatakiwa wasubiri dawa hadi zifike – ishara kwamba viongozi wao hawawajali. Waridi pia hawajibiki kazini mwake; anakuwa mkali kwa wagonjwa na pia anafuata kauli za wanasiasa bila kwanza kuzingatia maadili ya kazi yake: kuokoa maisha ya wagonjwa. Tatizo la njaa na umaskini linajitokeza wazi. Wananchi wanakula chakula cha mbwa na mabaki ya vyakula kutoka kwa matajiri. 

Onyesho La Pili
Onyesho la pili latokea nyumbani kwa Mstahiki Meya. Yuko mezani huku mbele yake kukiwa na mayai na chai pamoja na vyakula aina aina. Sakafuni kuna zuliaya kupendeza. Mandhari haya ni ushahidi tosha kwamba Meya anaishi maisha ya hali ya juu nay a shibe ikilinganishwa na watu wengine Jijini. Tunamwona Meya akilalamikia ‘viyai’ alivyopewa. Mazungumzo yake yote yanaashiria mtu mwenye maringo, kiburi na kutojali. Yeye analalamika juu ya udogo wa mayai ilhali wengine hawana hata hayo mayai. Anmwagiza Dida amwagize mwenye kuleta mayai hayo asiyalete tena. Pindi anaingiadaktari Siki, nduguye. Huyu anamtabulisha Meya kwetu kwa jina Sosi. Meya haelekei kupendezwa na jambo ili; hataki kuitwa ndugu Sosi, maana eti yeye sasa ni Meya. Siki amekuja kwa Meya kumjulisha hali ilivyo kwa wananchi na haswa kuhusiana na ukosefu wa dawa na ukosefu wa fedha za kugharamia matibabu. Badala ya kutilia maanani maswala haya, Meya anajitia hamnazo na kuanza kusifu baraza lake kama baraza bora zaidi. Siki anamkosoa haswa kwa kujilinganisha na majirani dhaifu. Anapendekeza kuzingatia ubora zaidi ya ubora wa majirani zao. Anazidi kumsimulia Meya juu ya matatizo ya watu wao; anamwabia watu wanakufa kwa njaa na ukosefu wa mahitaji ya kimsingi. Anamtahadharisha juu ya kuwaongoza watu wenye njaa. Meya anasisitiza kwamba, wenye kumchagua ni wengi na watazidi kumchagua. Anamwambia Siki kwamba akili ni mali. Ili kuthibitisha hayo, anamwagiza Gedi kupeleka ujumbe unaoagiza idhaa ya baraza kucheza nyimbo za uzalendo kabla na baada ya vipindi maarufu. Siki anashangaa kama kwamba watu watashibishwa na nyimbo hizo na kusema kuwa, hamna haja kuwapigia watu nyimbo za uzalendo miaka hamsini baada ya uhuru. Siki analalamikia swala la maendeleo akisema, wanatembea lakini hawaendi mbele, waenda kinyumenyume. Anamkumbusha Meya kwamba, afya bora nay a bure kwa wananchi wote ni moja kati ya malengo ya mji katika mpango wake wa maendeleo ya miaka kumi. Meya anasema kwamba wao wako na malengo ya kimaendeleo ya millennia na kwamba huo ndio muhimu. Adadai kwamba wameshaingia katika kiwango cha kimataifa na kupinga hayo ni kama kumkama samba mwenye watoto. Siki anamkumbusha kwamba, kufikia kumi sharti kuanza na moja; kwamba kumi haifikiwi katika ombwe tupu (vacuum.) Meya anaudhika na kumwagiza Gedi kumtoa nje Siki. Kasha anaagiza asilikaribie jingo lake tena bali alione paa. Meya anaagiza kuwe na mkutano wa dharuru ofisini bila ya mwanakamati yeyote kukosa.

Tathmini 
 Onyesho hili linamwangazia Meya kama mtu asiyejali maslahi ya wananchi aongozao. Wao wana njaa naye ana shibe kuu kufikia kiwango cha kuangalia udogo na ukubwa wa mayai. Hajali hali za watu wake, haswa juu ya umaskini, njaa na maradhi. Anapoambiwa kuna mtoto aliyekufa kwa njaa, anasema huyo ni mmoja na kwamba wamebaki wengi wanaomuunga mkono. Tofauti yajitokeza wazi kati ya ndugu wawili, Siki na Sosi. Siki ni mwenye utu ilhali Sosi ana ubinafsi mwingi na kiburi. Tofauti za kitabaka zinaonekana huku watu wa tabaka la juu wakiwa wanaishi maisha ya raha nao wa tabaka la chini wakiubeba mzigo mzito wa hali ngumu ya maisha; njaa na maradhi.



Onyesho La Tatu
Katika onyesho la tatu, madiwani watatu wako ofisini kwa meya. Wameketi wakiwa wanamsubiri meya. Madiwani hao ni: kinara wa Masuala ya Usalama, kinara wa Uhusiano Mwema, na wa Uchumi na Kazi.
Wamngojapo Meya, wanazungumzia maswala kadha; wanajadiliana kuhusu hali ngumu ya maisha kwa wananchi. Diwani I na DiwaniII wanaonekana wazi kutojali maslahi ya wananchi ilhali DiwaniIII anawatetea, pia ana maono. Anasisitiza kwamba watu wanataka vitendo bali si maneno. Wenzake ambao ni Diwani I na Diwani II waona kwamba, kuwepo kwao katika baraza ni bahati kubwa na kwamba jukumu lao ni kulitetea Baraza la Mstahiki Meya.
Diwani III anawaambia wenzake kwamba, kuna kufaa na kujifaa, akiwa na maana kwamba, baadhi ya madiwani wanatumia fursa yao kama viongozi kujifaa badala ya kuwafaa waliowachagua.
Meya ajapo, anawapeleka moja kwa moja hadi kwenye ajenda ya mkutano wao. Anasema kwamba, baadhi ya madiwani wanawachochea watu kuwa Baraza limeshindwa kutimiza majukumu yake. Anadai kwamba, hata miongoni mwa walio katika mkutano huo wao, wanawachochea wananchi.
Meya anwagiza kinara wa Usalama kuchukua hatua. Diwani I ambaye ni kinara wa Usalama anamhakikishia kwamba atawaamrisha vijana wa usalama (askari) kulilinda Baraza. Meya anmwambia kwamba mara hii hataki kusikia mtu amekufa, anamwagiza Bwana Uhusiano Mwema kuhakikisha kwamba ulimwengu haujui kwamba wanatumia askari kuwadhulumu wananchi.
Diwani I anaomba vijana kuandaliwa tamasha za nyimbo ili kuimarisha uzalendo. Anasema watatunukiwa zawadi ndogo ndogo na kuonyeshwa katika vyombo vya habari.
Diwani II –Bwana Uhusiano Mwema anatoa hakikisho kwamba mashondano haya yatapeperushwa moja kwa moja kupitia vyombo vya habari ili uzalendo uwamiminikie watu katika pembe zote za Cheneo.
Diwani III anasema kwamba, uzalendo hauji kwa watu kuimbiwa nyimbo bali kwa kujibu vilio vyao. Analalamika kwamba watu hawana ajira, na wale wenye ajira, hawapati mishahara ya kutosha. Pia wamelazimishwa na kaka zao (wazungu) wanawalazimisha kupunguza idadi ya wafanyakazi. Pia wazungu hawa hawajatoa hela za mkopo na kwa hivyo wafanyakazi hawawezi kuongezwa mishahara. Anaendelea kusema kwamba watu wana njaa na wanahitaji dawa na dawa zenyewe haziko. Tunakuja kufahamu kwamba dawa hizi haziji asilani.
Diwani III anendelea kusema kwamba ahadi za uwongo zitachochea ari ya watu. Meya anasema wakigoma, watafutwa na wengine wasio na kazi wataajiriwa.
Diwani II anapendekeza kuwe na kamati za kuhudumu ili kupunguza joto la malalamiko. Diwani I anapendekeza madiwani wanaowaunga mkono wawe viongozi wa kamati hizo.
Diwani II na Diwani I wanapendekeza nyongeza za mishahara kwa walinda usalama na madiwani. Diwani III anapingwa kwa kusema kwamba hamna fedha za kutosha. Pia anapendekeza madiwani walipe kodi kinyume na pendekezo la Meya kwamba wasilipe. Hatimaye, Meya anaamuru madiwani wasitozwe kodi kwani wana mzigo mkubwa wa kulihudumia Baraza.


Tathmini.
Katika onyesho hili, tuaona uozo ulioko katika Baraza. Viongozi wengi wanajifikiria wao pekee huku wakitumia walinda usalama kuwanyanyasa na kuwanyamazisha wananchi. Wafanyakazi hawapati mishahara ya kutosha huku viongozi wakikataa kulipa kodi.


SEHEMU YA PILI
Onyesho La Kwanza

Onyesho hili linatokea ofisini kwa Meya. Meya anajiandaa kwa mukutano wa mameya kutoka nchi za nje.
Katika maandalizi haya, anapanga kuwapa mapokezi ya kupigiwa mfano. Watakaa katika hoteli ya kifahari na kula vinono. Mvinyo utaagizwa kutoka Urusi na divai kutoka Ufaransa.
Rafiki yake, Bili, anamtembelea. Kutokana na mazungumzo yao tunajua kwamba ni marafiki wa jadi, na kwamba, Bili ni mshauri wa Meya na ndiye alimsaidia kufika alipo sasa.
Wazungumzapo pia, tunagundua kwamba mkewe Meya yuko ng’ambo alikoenda kuwatemeblea wanawe na pia kujifungua mtoto mwingine. Wanawe Meya wanasomea nje ya nchi kwa sababu viwango vya elimu vya huku kwao ni vya chini; mkewe atajifungulia ng’ambo kwa kuwa wakunga wa huko ni wa hali ya juu wakilinganishwa na wa huku kwao.
Swala la kandarasi linazuka ambapo Meya amefikishwa mahakamani na mwanakandarasi kwa kutoheshimu mkataba. Bili anamshauri amhimize mwanakandarasi kwenda mahakamani na akiri makosa yake ili Baraza limlipe fidia kasha wagawane pesa hizo.
Waendeleapo na mazungumzo na mipango yao, zinasikika nje, sauti za wafanyakazi wakilalamikia dhuluma na kusema wamechoka.anaarifiwa na Gedi kwamba wafanyakazi wanadia mishahara zaidi naye Meya anatishia kuwafuta kazi. Hatimaye anaamua kutafuta msaada kutoka kwa muhubiri.

Tathmini
Onyesho hili laonyesha uozo katika uongozi wa Jiji la Cheneo. Viongozi wanajua viwango vya elimu na vya afya viko chini na badala ya kuviinua, wanawapeleka watoto wao ng’ambo na kuwaacha wale wa maskini wakiteseka. Mabibi zao wakitaka kujifungua wanapelekwa nje.


Onyesho La Pili
Onyesho hili latokea katika ofisi ya Siki. Mwanzoni, tunamwano akiongea kwa simu na yaelekea anazungumza na Tatu –mmoja wa wawakilishi wa wafanyakazi wa Baraza la mji.
Tena anjisemea mwenyewe kwa mtindo wa kishairi akisemwa kwamba aliwaonya viongozi lakini hawakumsikia. Anasema kwamba, watu wenye njaa wamewaangusha watu wengi wenye nguvu na madaraka.
Pindi Waridi anaingia na kumwarifu nia yake ya kujiuzulu na kuacha kazi kwa vile haoni manufaa yake. Ameafikia uamuzi huu baada ya ya mtoto wa mamake mdogo kufia mikononi mwake.
Siki anamshawishi asiache kazi kwa matumaini kwamba mambo yatakuwa mazuri karibuni, pia kwa vile wagonjwa wanawahitaji, si kuwapa dawa bali matumaini na kuwa pamoja nao hata ingawa kuwepo kwao hakuna tofauti na vivuli vya wagonjwa wenyewe.
Tatu hatimaye anaingia na kueleza malalamiko ya wafanyakazi na nia yao ya kususia kazi. Tatu analalamika kwamba wagonjwa wanakufa ovyo kwa kukosa dawa na kwamba wamekuwa wakijaribu kukutana na Meya lakini kila mara, diary yake huwa imejaa. Siki anaomba waendelee mbele hatua kwa hatua bila kukata tama. Kasha Siki anawapa wazo la kutumia fursa ya wageni wajao mjini ili kutoa rai yao kwa Meya. Anashauri wamwambie Meya kwamba hawatazingatia usafi wa mji, na kwa vile anatarjia mameya kutoka miji mingine, huenda akasikiliza kilio chao.
Tathmini
Wafanyakazi wamelemewa na mzigo mzito wabebeshwao na viongozi wao. Hili huwa halina budi kutoke katika jamii yenye dhuluma. Tunaona kwamba watu wenye njaa ni watu hatari kuongoza.



Onyesho La Tatu

Meya anaenda kwa muhubiri ili kuombewa. Tunamwona akiwa na upole usio wa kawaida. Anapoombewa, askari wawili pamoja na Gedi wanaingia ghafla na kuamuru kila mtu alale chini na kuinua mikono juu. Wanafanya hivi bila kujua Meya mwenyewe yuko pale. Hii inaonyesha namna ambavyo askari hapa wanawadhulumu wananchi wa kawaida. Wanapogundua kwamba Meya alikuwa pale, wanaomba radhi na kusema kwamba, walisikia kelele na kudhani kwamba vinyangarika walikuwa wanaleta vitina yao.
Hatimaye Meya anaomba msamaha kutoka kwa muhubiri. Kasha anamwomba awe akipeleka maombi kwa Baraza mara moja kwa juma. Anaahidi kwamba, mhubiri atakuwa akipewa pesa za petroli na kupata sadaka ya laki moja kila mwezi.


Onyesho La Nne
Nyumbani kwa Diwani III(Bw. Kheri, Kinara wa Uchumi na Kazi), Siki amemtembelea. Ameenda huko kufuatilia maswala kuhusu wafanyakazi na matatizo yao.
Siki anamuuliza Kheri ni kwa nini hajamshauri Meya kutenda mambo inavyompasa. Kheri anasema kwamba, amejaribu sana kumshauri Meya lakini haelekei kumsikia. Anasema kwamba, Meya anakabiliwa na vikwazo mbalimbali; amelewa na mamlaka na hasikii ushauri, kazungukwa na washauri wapotovu wenye tama kubwa na njaa, Meya ana uwezo mkubwa vile vile, raia hawajahishwa katika utatuzi wa matatizo ya uongozi.
Kheri anasema kwamba hatakata tamaa na ataendelea kumshauri Meya. Pia anawalaumu wapiga kura kwani ndio huwachagua viongozi wabaya; anasema kwamba, hata uchaguzi ukifanywa sasa, matokeo hayatakuwa tofauti sana. Anasema, “…Mtu huvuna alichopanda…”
Siki anasema kwamba siasa ni  mchezo mchafu naye Kheri anasema kuwa anayeliogopa tope hawezi kujua njia nzuri ya kulisafisha.
Maswala ya uongozi mbaya pamoja na unyakuzi wa ardhi yanajitokeza hapa. Pia tunafahamishwa kwamba, Umeya hauna pato kubwa lakini ofisi hiyo iko na mianya mingi ya kujipatia utajiri.
Harufu mbaya ya taka katika mji inasemekana kama kiwakilishi cha uoz ulio ndani.

Tathmini
Katika onyesho hili, wahusika wawili waadilifu Dkt. Siki na Bw. Kheri wanakutana. Kulingana na mazungumzo yao, ni wazi kwamba wanayafikiria zaidi maslahi ya wananchi wa kawaida.   


SEHEMU YA III
Onyesho I
Katika ofisi ya Meya.
Diwani III ameitwa na Meya ilii kupewa agaizo la kuwaongezea madiwani mishahara. Zaidi ya kuwa wakati wa kuitayarisha mishahata umepita, Diwani III anasema kwamba, hakuhusishwa katika kikao kilichoidhinisha ongezeko hilo. Anaendelea kusema kwamba, wafanyakazi wamegoma kwa kutaka nyongeza ambayo hawakupewa. Vile vile, uwezo wa baraza ni mdogo hivi kwamba kuwaongezea madiwani mishahara kutaleta mivutano.
Meya anamlalamikia Kheri kwamba siku hizi haelekei kukubaliana na jambo lolote siku hizi.
Meya anadai kuwajua wanaogoma na kwamba ana uzoefu mkubwa wa mambo katika baraza na kungekuwa na vyeti hii leo angekuwa na Phd. Diwani III anapendekeza wafanye kazi yao vizuri kwa minajili ya kesho na vizazi vijavyo. Meya haoni hiki, alitakalo ni kuendelea kutawala na kunyakua mali. Anaamuru madiwani wapewe nyongeza bila ya kujali malalamiko ya wafanyakazi.

Tathmini
Onyesho hili linaakisi mabavu yanayotumiwa na Meya katika kuliendesha baraza. Anatumia nafasi mamlaka yake kutoa maagizo ya kuwapendelea madiwani wenzake huku akiwapuuza wafanyakazi.

Onyesho II
Meya yuko ofisini mwake. Sauti za wafanyakazi zinasikika wakidai haki zao. Kiongozi wao anawahutubia na kuwahimiza kudumisha umoja katika kupigania maslahi yao. Mara inasikika milio ya risasi na vilio vya watu wakikimbilia usalama wao. Meya anawacheka wafanyakazi kwa kutoroka. Bili, Diwani I na Diwani II wanaingia na wanafanya mazungumzo pamoja na Meya kuhusu yaliyotokea. Wanaelekea kulifurahia sana jambo lililotendeka la wafanyakazi kutawanywa na polisi.
Wanapanga kusubiri siku tano hivi wawaone wafanyakazi wakirudi kuomba kurejeshwa kazini. Diwani II anasema kwamba wawasukume wafanyakazi hadi wajue kwamba wao ni wananchi na kuna wenye nchi.
Hawa wane, kwa kufuata ushauri wa Bili, wanapanga kuuza Fimbo ya Meya iliyotengenezwa kwa dhahabu. Wanapanga kuuza Fimbo hii nje ya nchi huku wakidai iliibiwa wakati wa fujo za wafanyakazi.

Tathmini
Katika onyesho hili, tunaonyeshwa namna ambavyo wafanyakazi wanadhulumiwa kwa kupigwa na askari pindi wanapodai haki zao. Vile vile tunaona viongozi amabao hawajali maslahi ya wafanyakazi. Zaidi ya yote, tunawapata viongozi wawa hawa wakiiba raslimali za umma ili kujinufaisha wao weneyewe.


Onyesho III

Onyesho hili linaonyesha mhusika Dida ambaye anafanya kazi kwa Meya. Anaigiza namna ambavy wafanyakazi walifurushwa na polisi pale walipogoma. Anaanza maigizo yake kwa kusema: Duniani kuna watu na viatu
             na cheneo ina watu na viatu
anamlinganisha mfanyakazi wa kawaida na askari na kusema kwamba, askari na bunduki ni mfalme, ilhali mwenye kufagia anatukanwa na Bwana na kudhalilishwa. Anakejeli hali katika Jiji la Cheneo na nama wazee walivy
otimua mbio hata kuliko vijana ili kuokoa nafsi zao.
Anakejeli zaidi na kusema kwamba, hayo yamhusu nini na bora mameya wawepo ili apate watu kuwanadhifia nyumba.

Tathmini
Mwandishi anamtumia mhusika huyu kuikejeli hali ya mambo katika Jiji la Cheneo. Anatupatia mtazamo wa mwandishi kuhusu uovu unaotokea Cheneo.


Sehemu ya Nne

Onyesho I
Onyesho hili linafanyika ofisini mwa Meya, siku moja kabla ya kufika kwa wageni. Meya anakutana na wawakilishi wa wafanyakazi. Wawakilishi hawa wanatetea haki za wafanyakazi pamoja na nyongeza zao za mshahara.
Meya anashughulika zaidi na wageni wajao ilhali Baraza halijaweza kuwalipa wafanyakazi wao waliogoma. Meya anawaomba wasubiri wamalize na shughuli za kuwapokea wageni na waache kutoa vitisho. Wafanyakazi nao wanataka kutumia nafasi hii ya kuja kwa wageni ili kuitisha nyongeza ya mishahara. Wanatisha kutosafisha Jiji ili wageni wajapo wapate likiwa chafu na lenye uvundo.
Wawakilishi wa wafanyakazi wanataka kushirikishwa katika kikao cha Baraza ili watetee maslahi ya wafanyakazi lakini wanaambiwa hilo haliwezekani.

Wawakilishi wa wafanyakazi wanasisitiza kwamba mgomo utaendelea. Hawatashughulikia usafi wa Jiji na tishio la kipindupindu litakuwa halisi.

Tathmini
Onyesho hili laonyesha msimamo wa wafanyakazi wa kupigania haki zao pamoja na ule wa Baraza wa kutolegeza msimamo wake wa kuwanyima nyongeza ya mishahara. Tokeo lake ni kuendelea kwa mgomo. Hali hii inaakisi hali halisi katika mataifa mengi ya Kiafrika ambapo wafanyakazi wagomapo, hutishwa na kusitiziwa mishahara yao.


Onyesho II
Ofisini mwa Meya, siku moja tangu mkutano na waakilishi wa wafanyakazi. Meya anakutana na Diwani I na Diwani I. Meya analalamika kwamba, mambo hayakwenda walivyopanga. Wafanyakazi bado wako mgomoni. Jiji limejaa taka na harufu mbaya. Meya anaonekana mwenye wasiwasi kwa kuwa mambo hayakwenda walivyopanga. Wageni wanatarajiwa kufika siku hiyo ilhali wafanyakazi bado wamegoma. Kunatolewa pendekezo la kutumia kipasa sauti kuwatafuta vijana wa kufanya kazi ya kusafisha mji. Inatokea kwamba Bili ametoweka baada ya kumotosha Meya pamoja na madiwani wenza. Meya anajilaumu kwa kukosa kumsikiliza Bwana Uchumi na Kazi. Mara habari inafika kwamba wageni hawawezi kutwaa katika uwanja wao wa ndege na itabidi watue katika mji jirani. Jambo hili  lilimkera Meya sana kwa sababu  Shuara ni mji mdogo tu, pia wageni  wanaogopa kuambukizwa ugonjwa wa kipindupindu. Tunaona kwamba  mhazili  wa Meya naye achagoma.
Meya anaamrisha aitiwe askari lakini askari walikuwa wanakuja  kumjulisha safari ya wageni imeahirishwa  na na walikuwa wametumwa kutoka makao makuu kumshika yeye Meya  pamoja  na Diwani I na II ili  wakaeleze  maana  ya hali ilivyo Cheneo. Meya, Diwani I na II  wanawekwa  pingu mikononi.


MAUDHUI NA DHAMIRA

Dhamira ni funzo kuu litokanalo na kazi ya sanaa au lengo kuu la mwandishi.
Mwandishi wa tamthilia hii anaangazia swala la uozo katika uongozi. Anashughulikia ukosefu wa uwajibikaji wa viongozi katika jiji la cheneo.

Maudhui
Ubinafsi                       Kutowajibika
Umaskini                     Usaliti
Ufisadi                         Ulaghai
Unyanyasaji                 Migomo
Unafiki                         Mauti
Majuto                          Migogoro
Njaa                              Uzalendo
Uongozi mbaya            Maradhi
Uozo                             Vibaraka

1.      Uongozi mbaya
·         Ahadi  za uongo kuhusu dawa.
·         Swala la mishahara.
·         Viongozi wanakataa kulipa kodi.
·         Hawasikilizi maslahi ya watu.
·         Wanatumia polisi kuwanyanyasa watu.
2. Ubinafsi
Hii ni hali ya mtu kujifikiria zaidi ya watu wengine.
·         Watoto wa meya wanasomea ng’ambo ilhali elimu katika jiji la Cheneo iko chini.
·         Meya analalamika kuhusu viyai vidogo ilhali weungine hawana cha kukula.
·         Viongozi wajiongeza mishahara.
·         Viongozi hawalipi kodi.
·         Viongozi wanafikiria kuhusu maslahi yao pekee.

3. Ufisadi
Ni hali ya kujipatia mali kwa njia isiyofaa.
·         Meya alikuwa amepelekwa kortini lakini Bili anamwonyesha jinsi watakavyoiba pesa za mwanakandarasi.
·         Walinyakua ardhi.


4. Njaa
Hali ya ukosefu wa chakula.
·         Watu wanakufa kwa sababu ya njaa.
·         Mtoto alifariki kwa kukosa chakula/ lishe bora.

                                   5. Maradhi
·         Watu wanakufa kwa kukosa dawa.
·         Kuna tishio la kuzuka kwa maradhi kama kipindupindu.

6.Umaskini
·         Kuna ukosefuwa chakula dhidi ya umaskini.
·         Wagonjwa hawana pesa za kulipia madawa hospitalini.
·         Watoto hawasomi kwa sababu ya umaskini, hawana pesa za kulipa karo.

                                    7. Unyanyasaji/dhuluma
·         Watu wanalipa kodi ilhali viongozi hawalipi.
·         Wafanyakazi wanapogoma wanapigwa na askari.

                                    8. Unafiki
Hali ya mtu kujifanya mzuri ilhali ni kinyume yake.
·         Meya anaombewa na mhubiri na pia kumwahidi kumlipa.
·         E Meya akizungumza na Bili anajifanya mzuri.
·         Anajifanya mkarimu akishughulika wageni watakunywa nini.

                                     9. Kutowajibika.
·         Hawalipi mishahara ya wafanyikazi.
·         Hawasikilizi vilio vya watu.

                                      10. Migogoro
·         Mgogoro dhidi ya meya na madiwani,viongozi dhidi ya viongozi.
·         Mgogoro kati ya viongozi na raia inajitokeza kwa njia ya migomo/vitisho.
·         Meya na nduguye Siki.
·         Kati ya viongozi na wanataluma,ambapo viongozi wanataka kuwageuza kuwa wanasiasa.

                                            11. Uozo
Kuharibika kwa mambo.
·         Wagonjwa wanaacha hospitalini bila dawa.
·         Hali iya watu kufa kwa njaa ilhali viongozi wanajifikiria wao wenyewe.
·         Viongozi hawashughuliki na elimu ya watoto wa wananchi.
·         Meya ananyakua viwanja vya ardhi na kuuza ili kujitajirisha.
·         Viongozi wanapanga kuuza fimbo ya meya ya nchi.
·         Meya anapotuma askari kuwachapa wafanyikazi wanapogoma.


              12. Vibaraka.
·         Ni wale watu ambao hufuata viongozi kwa upofu na kuwasifu hata wakifanya mabaya.kwa mfano Diwani I na II.

                                                  13. Uzalendo
                                                      Hali ya mtu kuipenda nchi yake kwa dhati.
·         Diwani III anatetea wafanyikazi na hakumbaliani na maamuzi yanayotolewa.Pia analihurumia jiji.
·         Sili anawahudumia wagonjwa na kuwatetea wafanyikazi.


                                                       14. Usaliti
·         Ni kumtendea jambo ambalo ni kinyume kabisa na imani yake.
·         Meya anasaliti jiji lake.
·         Viongozi wanawasaliti wafanyikazi kwa kujiongeza mishahara.
·         Wanatekeleza usaliti kwa;
-Kutoimarisha uchumi.
-Hawajaimarisha nafasi ya ajira.
-Kuimarisha elimu na afya.
Badala yake wanafanya yafuatayo;
·         Viwango vya elimu na afya vyaenda chini na wao wanatafuta hizo nje ya ndani.
·         Wanajiongeza mishahara mara kwa mara wanapokutana kwa kupora pesa za wananchi na kunyakua ardhi.


                                           15. Ubadhirifu
Ni matumizi mabaya ya pesa.
·         Wageni wanapokuja wanapangiwa dhifa kubwa na kukaa kwenye hoteli ya bei ya juu na pia kuagiziwa mvinyo kutoka nchi za nje.
·         Wanaomba marupurupu na meya anakubali.
·         Meya anapanga mhubiri awe anapewa pesa kila mwezi ili kumvutia.
·         Madiwani wanaongezwa mshahara kiholelaholela.

                                       16. Usugu
Ni hali ya mtu kusikia wala kukubali ushauri.
·         Meya amejaribiwa kuzungumziwa na Sili ilhali anakataa kuyasikia anayosema.


                                    17. Majuto
                                        Ni masikitiko kwa jambo ambalo limetokea.
·         Diwani I na II wanajuta kwa kukubaliana na Meya kuleta uozo katika jiji la Cheneo.

                                    18. Ulaghai
                                       Hali ya kumnyang’anya mtu mali kwa kuutumia ujanja.
·         Meya anawaongezea viongozi mishahara ilhali wafanyikazi wanadai kuongezwa mishahara lakini Meya anawaambia kuwa hakuna pesa.

                                    19. Migomo
·         Ni hali ya wafanyikazi kukataa kufanya kazi hadi masharti fulani yatimizwe.
·         Wafanyikazi walipogoma wakidai kuwa waongezwe mishahara yao .

                                   20. Mauti
Ni hali inayomfanya kiumbe kukosa uhai.
·         Wakati ambapo mtoto wa mamake mdogo Waridi alikufia mikononi mwake.
·         Tatu alipokuwa analalamika kuwa wagonjwa wanakufia hospitalini kwa kukosa dawa.

WAHUSIKA
1.Meya Sosi
                                     Ndiye Meya wa jiji la Cheneo.
                                     Ni ndugu wa daktari Siki na rafikiye Bili.
Sifa zake
1.      Ananyakua ardhi
Ni mwizi-alikuwa amepanga kuiba fimbo ya Meya na kuiuza.
2.Ni mwenye ubinafsi.
Anajifikiria yeye mwenyewe, analalamika kuwa viyai ni vidogo, ilhali wengine hawana chakula.
Wanajiongeza mishahara lakini hawaongezi mishahara ya wafanyikazi.

3.Ni msaliti.
Amewasaliti wananchi kwa kutowajibika katika kazi yake ya uongozi.

4.Ni mtu sugu.
Kwa kuwa hafuatilii ushaurianaopewa na nduguye Siki.

5.Ni Mlaghai.
Amenyakua ardhi na kuiuza kwa manufaa yake mwenyewe.

6.Ni mwenye majuto.
Anajuta kwamba mambo yanakwenda kinyume na alivyotarajia.

7.Ni mnafiki.
Anajifanya mwema kwa mhubiri na kutoa sadaka kanisani ya laki moja.

8.Ni mwongo kwani anadanganya kuwa dawa ziko ilhali hakuna.

9.Hana utu
Hii ni kwa sababu alipoambiwa kuwa motto mmoja alikufa hakujali na kusema kuwa ni mmoja tu.

10. Ni mnyanyasaji.
Wafanyikazi wanapogoma, anatumia polisi kuwapiga wananchi.

11. Ana upeo finyu.
Haoni mbali.Hakufikiria jinsi mambo yatakavyoenda mrama.

12. Ni mtovu wa uzalendo.
Hashughuliki na wafanyikazi  na taasisi ya elimu ya jiji la Cheneo.

13.Ni mtu mjinga,
Alidanganywa na Bili hadi mambo yanakwenda mrama.

14.Ni mtu mwenye majivuno.
Hawezi kula vile viyai vidogo.

       Umuhimu
·         .Ni kielelezo cha upotovu katika jamii.
·         Anaonyesha ubinafsi na mivutano na kutowajibika miongoni mwa viongozi.
·         Kupitia kwake tunaona mwandishi akionyesha uongozi mbaya.


2 .Diwani III

Sifa
1.Ni mwadilifu.
·         Ni mtu mwenye maadili mwema.
·         Anapinga mambo mabaya ya Meya.
2.Ni mnyenyekevu.

·         Alidumisha heshima ya Meya ingawa alijua kuwa ni mwizi.

3.Ni mtu asiye na tamaa.

·         Hana tamaa ya kuongezwa mshahara na anapinga baadhi ya uamuzi unaofanywa na wengine.

4.Ni mzalendo.
·         Anawashughulikia wananchi na anataka viongozi wenzake walipe kodi.

5.Ni mwenye subira.
·         Amemshauri Meya lakini haonyeshi mabadiliko.

6.Ana ushauri mwema.

Umuhimu.
1.Ni mpinzani mkubwa wa maovu katika jamii.

3.MadiwaniI na II.
·         Ni mabarakala wanaotenda mambo ili kumfurahisha Meya Sosi.
·         Ni mwenye tamaa.Wanataka nyongeza ya mishahara bila kujali wananchi na wanakataa kulipa kodi.
·         Wanapenda mizengwe(mipango ya kisirisiri)bila kumhusisha diwani III
·         Ni waongo.Wanawadanganya wananchi juu ya madawa na kuhusu nchi.
·         Ni watu wenye njama.Wanapanga kuuza fimbo ya Meya.
·         Hawana msimamo imara.Hawashikilii mambo,wanafuata amri za Meya bila kuuliza maswali.
·         Ni wajinga.wanasaliti wananchi waliowachagua.

4.Siki.
Ni daktari katika zahanati ya jiji la Cheneo.

Sifa
1.Ni mwadilifu-anawashughulikia wananchi.
2.Ni mwenye bidii.
3.Mwenye ushauri nasaha.
4.Mtulivu.
5.Ni mtu mbaraza.
6.Mkereketwa.

5. Bili 
Ni rafiki yake Meya.

Sifa
I.Ni mbunifu
2.Ni mjanja
3.Ni mpotovu
4.Ni mwenye tama
5.Ni mnafiki


6.Tatu
Ni mwakilishi wa wafanyikazi.

Sifa
1.Ni mtetezi mkali wa haki na maslahi.
2.Ni jasiri.
3.Ni mbaraza.
4.Ni mnafiki.

Mtindo na matumizi ya lugha
1.Kinaya.
2.Methali.
3.Sajili ya dini.
4.Kuchanganya ndimi.
5.Tashbihi.
6.Semi.
7.Uzungumzi nafsia.

1.      Kinaya.
Ni hali ya mambo kutokea kinyume na matarajio.

Mfano:
·         Tamthilia hii inaonyesha kinaya wakati ambapo Meya alikuwa anawaambia wagonjwa wasubiri dawa eti kwamba zitakuja baada ya siku tatu ilhali hakuna dawa zozote.
·         Kinaya kinajitokeza tena pale ambapo meya anajifanya mzuri kwa mhubiri anapoenda kumwomba msamaha.Pia anaahidi kuwa mhubiri atakuwa akipewa pesa za petroli na kupata sadaka ya laki moja kila mwezi.
·         Pia tunaona kinaya katika tamthilia hii wakati ambapo Meya alikuwa anateta kuhusu viyai vidogo ilhali wengine katika jiji la Cheneo hawana chakula.


2.Methali
 Ni kifungu cha maneno yanayotumiwa pamoja kisanii kwanjia ya kufumba au kupigia mfano.
Mifano:
1.Ngoja ngoja huumiza matumbo.
·         Hii methali inatumiwa katika hadithi hii kueleza kwamba jambo linalostahili kutendwa papo hapo lisipotendwa kwa wakati ufaao,hutia hasara.
·         Methali hii ilitumiwa na Siki wakati ambapo alikuwa akimweleza Waridi kuwa wagonjwa wanasubiri dawa ziwasili,ugonjwa nao hautasubiri.

2.Haraka haraka haina Baraka.
·         Maana ya methali hii ni kuwa jambo lifanywalo haraka haraka haliwezi kufana,sharti liende kwa mpango wa taratibu.
·         Methali hii ilitumiwa na Waridi kumwambia Siki huwa asiwe na haraka ya kuwashughulikia wagonjwa kwani hawana hela za kulipia huduma za zahanati.

3.Dawa ya adui ni kummegea unachokula.
·         Methali hii ilitumiwa naBili kwa Meya juu ya kugawana fidia baada ya mwanakandarasi kuishtaki Baraza.

4.Wasemao mchana usiku watalala.
Maana;watu hata wakisema itafika wakati wachoke.Bili anaitumia methali hii kwa kurejelea sauti za wafanyikazi wanaogoma.

5.Ganga ganga za mganga huleta tumaini.
Kurukaruka kwa mganga huletea wagonjwa tumaini.Siki anaitumia methali hii kwa Waridi ili awaletee wagonjwa matumaini.

6.Mbiu za sakafuni huishia ukingoni.
 Ina maana kuwa mambo yaliyofanywa kwa giza yatafichuliwa.Bili anatumia kurejelea kwa wanahabari wanaotaka kuhoji Meya kuhusu mgomo.

7.Asante ya punda ni mateke.
Maana ya methali hii ni kuwa ukifanya mtu mema anakulipa na maovu.Meya anaitumia methali hii kwa mhazili wake aliyeacha kazi.

8.Msiba wa kujitakia hauna kilio.
Ina maana kuwa ukijiletea shida hauna mtu wakulaumu ila wewe mwenyewe.

9.Yaliyopita yamepita tugange yajayo.
Hii methali ina maana ya mambo yaliyopita yamepita tungoje yajayo.

10.Mpiga ngumi ukuta huumiza mkonowe.
Hii methali ina maana kuwa ukifanya mambo ukidhani unawaumiza wengine,wajiumiza wewe mwenyewe.

MBINU YA KUCHANGANYA NDIMI.
Hii ni hali ya kutumia lugha nyingine isipokuwa lugha yenye hadithi imeandikwa nayo. “What do you think this is?food poison.
·         ”Ooh yes”I understand.
·         “Collective responsibility.
·         “Yes sir”(Gedi).

Tashbihi.(pg 47,48,45,14,34,69).
Hali ya kulinganisha vitu na maneno ya ulinganishi kama vile kama,mithili ya.kwa mfano;
·         Kumkunja kila aliye chini yake kama ua wakati wa alasiri –Diwani wa III ndiye aliyenena haya kwa siku kuwa Meya ana uwezo.
·         Ni kama mtoto na chakula-DiwaniIII ndiye aliyenena haya kwa Siki kumwonyesha kuwa cheo kinaweza levya mtu asahau alipokuwa jana.
·         Kushindana naye ni kama kushindana na ndovu-Diwan III aliyanena haya kwa Siki kumwonyesha kuwa Meya ana mamlaka makubwa.
·         Inasimama kama ya mtende –Ni Siki aliyoyasema maneno haya  kwa Diwani III kwani hakutarajia kumpata kwake na bahati yake akailinganisha nay a mtende.
Mimi na Menga  ni mfano wa mfano wa mafuta na maji-Siki anamweleza DiwaniIII kuwa yeye na Meya ni mfano wa mafuta na maji,kwani hawajali kubaliana kwa maswala mbalimbali.
·         Kumpiga haya ni sawa na kumkama simba mwenye watoto.Haya ni maneno ya Meya aliyoyanenea Daktari Siki kuwa akipinga malengo ya kimaendeleo ya milenia ni hatari kwani ni kama kumkamua samba mwenye watoto.
·         Amekufa kama nzi-Beka ndiye aliyenena maneno haya kwa Meya;kifo cha mtoto wa Kerekecha alikufa kililinganishwa na kifo venye nzi hufa ovyo.

Misemo.



Mifano.
·         Watu sasa wanatumbua mbivu na mbichi-Huu msemo ulinenwa na DiwaniIII kwa DiwaniI na DiwaniII kuwa hakuna geni ambalo watawaambia watu kwani wanayafahamu yote.
·         Ndiyo huko kuwaua ndege watatu kwa jiwe moja.Huu ni msemo wa Meya kwa Bili ambapo Bili kamwambia kuwa kandarasi mpya yategemea kauli yake.
·         Msikate tamaa-Huu ni msemo wa Siki kwa Tatu kuwa wasikate tamaa kushinikiza kumwona Meya.
·         Aliyeliogopa tope kummwangikia hawezi kujua njia nzuri ya kulisafisha-DiwaniIII ndiye aliyesema msemo huu kwa Siki.

Mdokezo.
Ni mbinu ya kukatiza msemo.
Km.Amesema mwenyewe Meya….Haya ni maneno ya Waridi kwa Siki akimweleza kuwa dawa zaja.
Na leo…Afadhali jana.Haya ni maneno ya mama mwenye mtoto mgonjwa kwa Siki kumweleza hali ya mtoto wake.
Lakini daktari ha…Haya maneno ya Waridi mama kwa Siki kumwambia mama mwenyewe hana pesa za kulipia huduma zao.
Hata huhitaji wakili…Haya maneno ya Bili kwa Meya kuhusu ile kesi ya mwanakandarasi.Ni kama…..ni kama…Talk of devil…Haya ni maneno ya Bili kwa Meya.
Lililoandikwa….Haya ni maneno ya DiwaniIII kwa Siki.
Ni…ni…ni…Haya ni maneno ya Gedi akitaka kumwarifu Meya habari kuwa wanauwanja wamegoma.

Sitiari/Jazanda


Kwa mfano.
·         Unamkanya nyoka mkia.
Maneno haya yalisemwa na Siki akimwambia Meya kuhusu mambo yangemgeuka na kuharibika kwa kutowashilikisha watu katika mipango ya baraza.
·         Watu sasa watafahamu mbivu na mbichi.
Maneno haya yalisemwa na DiwaniIII akiwaambia madiwani wenzake kuwa watu wanayaelewa mambo sasa.
·         Lazima kwanza mnihakikishie kuwa huyo sumu hapati hata tununu ya mambo hii.Hii ni bomu inaweza kutulipukia usoni.Maneno haya yalisemwa na Meya kwa DiwaniI na II wakati walipotaka kuiuza fimbo ya Meya.

Uzungumzi nafsi.
Hali ya mtu kuzungumza pekee/nafsi yake.km.

i)Dida.
-Anazungumza juu ya kazi ya askari.
Jambo la watu kukimbia mbio.

ii)Meya.
Baada ya mazungumzo na DiwaniIII anabaki kusema peke yake.(uk56)”….Nifikiri ninaweza kusikiliza viongozi wao si kila mtu!”

Tashtiti.
Mbinu ya kutumia vichekesho au dhihaka ili kufichua uovu Fulani.km
·         Kuna watu na viatu-Dida anaeleza uovu katika cheneo namna ya dhihaka.
·         Meya kutamka maneno ya kidini-Mwandishi anatumia njia hii kuashiria jambo fulani kama unafiki.
·         Daktari anatengeneza mchanganyiko wa maji ,sukari na chumvi.Anaonyesha mambo yameharibika kabisa.
·         Meya na marafiki zake wanashikwa na polisi-wakikuwa na mamlaka makubwa.

NAMNA YA KUJIBU MASWALI YA FASIHI.
Kuna maswali ya aina mbili katika fasihi;
-Maswali ya muktadha.
-Maswali ya insha.
a)Maswali ya muktadha.
Swali la muktadha huhusisha dondoo kutoka kitabuni ambapo mtahiniwa hutakiwa kuiweka dondoo hilo katika muktadha wake.Muktadha hapa ina maana ya mazingira ya kutokea kwa jambo.Katika kulijibu swali la muktadha mambo manne huhusishwa.
i)Mwenye kuyasema.
ii)Mwenye kuyambiwa.
iii)Mahali walipokuwa.
iv)Swala lenye lililokuwa likiendelea.

Km.Wewe wa ndani zaidi kuliko mimi…kama ni habari utakuwa unazipata kwa urahisi kuliko mtu wa nje…
Mwenye kuyasema maneno haya ni DiwaniIII.Alikuwa anamwambia Siki.Walikuwa nyumbani mwa DiwaniIII.Walikuwa wanazungumzia venye watamwona Meya kutetea maslahi ya watu wa Cheneo.

b)Maswali ya insha.
Maswali haya yanazingatia mpangilio wa aya.k.m.Taja na ufafanue maudhui kumi katika tamthilia ya Mstahiki Meya.
·         Utangulizi-Uwe mfupi wa kilenge moja kwa moja.km.katika tamthilia hii ya Mstahiki Meya.




 





13 comments:

  1. Ingawa ninampa mwenye fikra hii mkono wa Tahania ,ningependa mhusika wa hiki kifungu hiki azidikuujenga hadi Mwisho wa Mstaki Meya!...

    ReplyDelete
    Replies
    1. Shukrani Gallic Thomz. Mwongozo huu utakamilika hivi karibuni.

      Delete
  2. This comment has been removed by the author.

    ReplyDelete
  3. Je,unaweza kunieleza kwa ufaafu anwani hii'Mshtahiki Meya'?

    ReplyDelete
  4. anwani ya mstahiki meya ni kinaya jadili

    ReplyDelete
  5. Asante. Mwongozo wa Kidagaa Kimemwozea waandaliwa.

    ReplyDelete
  6. Heko wadadisi wa lugha kwa kazi murwa

    ReplyDelete
  7. Kazi nzuri hii inapendeza. Shukran'

    ReplyDelete